Monday, November 11, 2013

Uchaguzi Mkuu TBF Desemba 10

Na Mohamed Mharizo, Dar es Salaam:

UCHAGUZI mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Kikapu Tanzania (TBF), unatarajia kufanyika Desemba 10 mwaka huu jijini Mbeya.

Kwa mujibu wa Rais wa TBF, Mussa Mziya, uchaguzi huo unafanyika kwa mujibu wa katiba baada ya uongozi uliopo madarakani kumaliza muda wake.

“Napenda kuchukua fursa hii kutoa tangazo rasmi la tukio la uchaguzi mkuu wa viongozi wa TBF utakaofanyika Desemba 10 mwaka huu jijini Mbeya na kikatiba inabidi ufanyike uchaguzi kuwapata viongozi wapya watakaoendesha shughuli za shirikisho kwa miaka minne ijayo,” alisema.

Alisema uchaguzi huo utafanyika baada ya kumalizika kwa mashindano ya Taifa Cup, ambayo mwaka huu yanafanyika mkoani Mbeya kuanzia Novemba 30 hadi Desemba 8 jijini Mbeya.

Alizitaja nafasi zitakazowania katika uchaguzi huo ni Rais, Makamu wa Rais, Katibu Mkuu, Katibu Mkuu Msaidizi, Mhazini, Kamishna wa Mipango, Kamishna wa Ufundi na Mashindano, Kamishna wa Waalimu, Kamishna wa Watoto na Shule, Kamishna wa Wanawake, Kamishna wa Waamuzi, Kamishna wa Tiba ya Wanamichezo na Kamishna wa Walemavu.

Alisema taratibu zote za uchaguzi huo zitasimamiwa na Baraza la Michezo la Tanzania (BMT) ambao ndio watakaokuwa wakitoa fomu za maombi ya wagombea.

“Kwa niaba ya uongozi wa shirikisho napenda kuchukua nafasi hii kuwaomba wadau, wapenzi wa michezo na wananchi wote kwa ujumla wenye sifa na wanaopenda kuongoza wajitokeze kwa wingi kuchukua fomu za maombi ya uongozi, baada ya tangazo la BMT la kuanza kuchukua fomu hizo kwa nafasi zote zilizotangazwa,” alisema.

0 comments:

Post a Comment