Monday, November 11, 2013

Rekodi ya ufungaji yapanda Ligi Kuu

Kikosi cha Simba
Na Abducado Emmanuel, Dar es Salaam

CHATI ya ufungaji mabao katika Ligi Kuu ya Vodacom, imeonekana kupanda kwa kasi msimu huu kutokana na mabao 207 kufungwa hadi kumalizika kwa mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo tofauti na msimu uliopita.

Msimu uliopita baada ya kumalizika kwa mzunguko wa kwanza, jumla ya mabao 196 yalifungwa lakini msimu huu kuna tofauti kubwa kutokana na idadi ya mabao yaliyofungwa.

Timu za Simba, Mtibwa Sugar na Yanga ndizo zimepata ushindi mnono katika ligi hiyo, baada ya Simba kuifunga Mgambo Shooting mabao 6-0, Mtibwa Sugar iliifunga JKT Oljoro mabao 5-2, huku Yanga ikiifunga Ashanti United mabao 5-1.

Yanga ndiyo inayoongoza kwa kufunga mabao mengi ikiwa imefunga mabao 31, Simba inafuatia kwa mabao 26 na Azam FC imefunga 23, huku Mgambo JKT ndio timu iliyofunga mabao machache kwa kupachika wavuni mabao matatu.

Mshambuliaji wa Simba, Amisi Tambwe anaongoza kwa kufunga jumla ya mabao 10 akifuatiwa na Elias Maguri wa Ruvu Shooting aliyepachika mabao tisa. Hamis Kiiza (Yanga), Kipre Tchetche (Azam FC) na Juma Luizio (Mtibwa Sugar) kila moja amepachika mabao nane.

Kiiza amefikia rekodi yake ya msimu uliopita, baada ya kufunga mabao nane aliyofunga.

0 comments:

Post a Comment